Na Esther Mnyika, Dodoma
RAIS Dk. Samia Suluhu Hassan ameipongeza Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania ( TADB) Kwa utendaji mzuri ulioleta tija kwa wakulima nchini.

Ametoa pongezi hizo leo Agosti 8, 2025 Dk. Samia wakati wa kilele cha Maadhimisho ya Maonesho ya Kimataifa ya Kilimo Nanenane ambapo kitaifa imefanyika Jijini Dodoma yameshirikisha wakulima, wafugaji na wavuvi kutoka mikoa mbalimbali nchini.
Amesema utendaji mzuri wa benki hiyo umewapa uwezo wa kuwezesha wananchi na kuendelea kuwa mdhamini mkuu wa maonesho hayo kwa kipindi cha miaka mitano ijayo.
Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa TADB, Frank Nyabundege amesema mtaji wa benki hiyo umekua kutoka shilingi bilioni 60 hadi shilingi bilioni 442 pia amemshukuru Rais Dk.Samia kwa kuendelea kuwawezesha wakulima ka kuwapatia mikopo ya pembejeo.

“Rais umeitafutia fedha Benki hii kutoka kwa wahisani mbalimbali ambapo wakati unaingia madarakani hakukuwa na fedha kutoka kwa wahisani lakini tumepata shilingi bilioni 564 kupitia nguvu zako kutoka kwa wahisani mbalimbali katika diplomasia ya uchumi,”amesema.
Amesisitiza kuwa benki hiyo itaendelea kudhamini maonesho ya Kimataifa ya Kilimo Nanenane kwa kipindi cha miaka mitano mfululizo kwa sababu imiwezesha kuwa na mtaji mkubwa.
Nyabundege amesema wakati anaingia madarakani Rais Dk. Samia jumla ya mikopo ilikuwa shilingi trilioni 19 hadi kufikia Juni mwaka huu shilingi trilioni 42.
“Hii maana yake kwamba uchumi wetu unakuwa na hiyo ni kwasababu ulivyoingia madarakani uliamua kwenda kufanya mageuzi katika nchi yetu kupitia sekta ya Kilimo na ndio maana ukatupatia sisi mtaji, na sisi tutaendelea kudhamini maonesho haya,”ameeleza.



