Dar es Salaam
ALIYEKUWA Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) Mkoa wa Shinyanga, Emanuel Ntobi, leo Juni, 3 2025 amejiunga rasmi na Chama cha ACT Wazalendo.

Hafla ya kumpokea imefanyika Makao Makuu ya ACT Wazalendo, Magomeni, Dar es Salaam, na kuongozwa na Katibu Mkuu wa chama hicho, BAdo Shaibu.
Akizungumza na waandishi wa habari mara baada ya kukabidhiwa kadi na katiba ya ACT Wazalendo, Ntobi amesema uamuzi wake umetokana na tathmini ya kina aliyofanya kuhusu vyama mbalimbali vya upinzani nchini. Kwa mujibu wake, ACT Wazalendo ndicho chama pekee chenye uwezo wa kuiondoa CCM madarakani.
“Nimevutiwa na kiwango cha juu cha demokrasia ndani ya ACT Wazalendo. Demokrasia siyo tu kufanya uchaguzi, bali pia hali ya utulivu na mshikamano baada ya uchaguzi,” amesema Ntobi.
Pia ameeleza kuwa kauli mbiu ya ACT Wazalendo kuelekea uchaguzi mkuu, inayosema “Muhuni Hasuswi”, imemvutia na kumtia hamasa ya kujiunga ili kuongeza nguvu katika mapambano ya kisiasa dhidi ya mfumo wa utawala uliopo.
Kwa hatua hiyo Ntobi anakuwa mmoja wa viongozi waandamizi wa upinzani waliokihama CHADEMA na kujiunga na ACT Wazalendo katika harakati za kuimarisha upinzani kuelekea uchaguzi mkuu ujao.