MAKUMU Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi (CCM) Bara, Stephen Wasira amewaonya wanachama wa CCM na Watanzania kwa ujumla, wasidanganywe na kauli mbiu zinazotolewa na Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), ikiwamo kauli mbiu za No Reforms, No Election, Movement of Change (M4C) na No Hate No Fear.
Wasira amesema kuwa CHADEMA imekuwa ikitumia kauli mbiu hizo bila kutekeleza vitendo vya kuunga mkono kauli hizo, na kwamba hii ni tabia yao ya muda mrefu ya kujinufaisha kisiasa kwa maneno badala ya matendo halisi.
Kauli hiyo ameitoa leo, Juni 10, 2025, alipokuwa akizungumza na wanachama wa CCM na wajumbe wa Mkutano Mkuu wa Wilaya ya Tunduru, mkoani Ruvuma, katika ziara yake ya kikazi.
Amesisitiza kuwa CCM itaendelea kuwa chama thabiti chenye misingi imara ya utekelezaji wa sera na ilani zake kwa vitendo, tofauti na vyama vinavyotegemea kauli zenye lengo la kuchochea hisia za wananchi bila hoja madhubuti.
“CHADEMA wamekuwa mabingwa wa kutoa kauli mbiu kila jambo, lakini Watanzania sasa ni waelewa. Wasiwaamini, maana hawana ajenda ya maana zaidi ya maneno,” amesema Wasira.
Ziara hiyo inalenga kuimarisha uhai wa chama na kutoa miongozo kwa viongozi wa CCM katika ngazi ya wilaya, kujiandaa na uchaguzi wa serikali za mitaa na uchaguzi mkuu ujao.
Pia amewasihi watanzania wote wakiwemo wanachama na wapenzi wa Chama hicho kujiandaa kwenda KUTIKI kwa kumpigia kura mgombea urais wao Dk.Samia Suluhu Hassan pamoja na mgombea mwenza Dk.Emmenuel Nchimbi.