Kampala, Uganda
Rais wa Uganda, Yoweri Kaguta Museveni, amethibitishwa kuwa atawania tena urais katika uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika mapema mwaka 2026, hatua itakayoongeza muda wake wa uongozi uliodumu kwa takriban miongo minne.
Uthibitisho huo umetolewa kwa mara ya kwanza na chama chake tawala cha National Resistance Movement (NRM) kupitia kwa Mwenyekiti wa Baraza la Uchaguzi la chama hicho, Tanga Odoi, katika video iliyochapishwa Jumatatu jioni na shirika la utangazaji la UBC kupitia mtandao wa kijamii wa X (zamani Twitter).
Odoi alisema kuwa Rais Museveni, ambaye kwa sasa ana umri wa miaka 80, atachukua rasmi fomu ya kugombea urais kupitia NRM tarehe 28 Juni 2025, ikiwa ni hatua ya mwanzo kuelekea uchaguzi mkuu wa mwezi Januari 2026.
Museveni amekuwa madarakani tangu mwaka 1986 na anashikilia nafasi ya nne miongoni mwa viongozi waliotawala kwa muda mrefu zaidi barani Afrika. Katika miaka ya nyuma, chama chake kimefanya mabadiliko ya kikatiba ili kuondoa kikomo cha mihula na umri wa kugombea urais, hatua zilizomuwezesha kuendelea kugombea.
Uchaguzi huo ujao utahusisha pia uchaguzi wa wabunge, huku wachambuzi wa siasa wakiangazia mustakabali wa kisiasa wa taifa hilo la Afrika Mashariki linalozidi kukumbwa na mijadala kuhusu demokrasia na mabadiliko ya uongozi.