Na Mwandishi wetu, Zanzibar
MKE wa Rais wa Zanzibar, Msarifu na Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini ya Zanzibar Maisha Bora Foundation (ZMBF), Mama Mariam Mwinyi amekutana na ujumbe kutoka Equity Group Foundation ukiongozwa na Mwenyekiti wa Taasisi hiyo, Dkt. James Mwangi katika Ofisi za ZMBF, Migombani Mkoa wa Mjini Magharibi Juni,27 2025.

Katika mkutano huo umeangazia maeneo ya ushirikiano kati ya taasisi hizi mbili, huku ukitoa fursa ya kubadilishana uzoefu katika nyanja mbalimbali zinazohusu afya, elimu, lishe na uwezeshaji wa wanawake na vijana kiuchumi.

Aidha , Mama Mariam Mwinyi ameweka wazi dhamira ya ZMBF kuendelea kushirikiana na wadau mbalimbali kwa lengo la kuboresha Maisha ya Wazanzibari kwa kubainisha kuwa Taasisi ya ZMBF iko tayari kushirikiana na Equity Group Foundation katika kutekeleza miradi ya kimkakati katika sekta za afya, elimu na maendeleo ya kiuchumi.
Kwa upande wake, Dk. James Mwangi amesema amefurahishwa kuona maeneo mengi yanayofanana kati ya ZMBF na Equity Group Foundation, hasa katika kuimarisha lishe ya watoto wadogo na kuwawezesha wakulima wa mwani.

Ameeleza kuwa utayari wake wa kushirikiana na ZMBF katika kusaidia utekelezaji wa miradi hiyo kwa ufanisi zaidi.