Home KITAIFA Dk. Nchemba Aahadi Watanzania Wote Wanasikilizwa na Kuheshimiwa Katika Ofisi...

Dk. Nchemba Aahadi Watanzania Wote Wanasikilizwa na Kuheshimiwa Katika Ofisi za Umma

*Watanzania Wote Watasikilizwa na Kuhudumiwa kwa Heshima

*Ajira na Kupambana na Umaskini

*Dira ya Maendeleo ya Taifa 2025-2050: Ajira Milioni Nane kwa Vijana

Na Esther Mnyika, Dodoma

WAZIRI Mkuu Mteule wa Jamhuri ya Muungano wa  Tanzania, Dk. Mwigulu Nchemba  ameahidi kuwa serikali itahakikisha  kila Mtanzania  hususan wale wa ngazi za nchini  wanasikilizwa na kuheshimiwa kila ofisi ya umma. 

Akizungumza  leo Novemba,13 2025  Bunge jijini Dodoma  baada ya kuthibitishwa  na Bunge  Dk. Nchemba  amesema  serikali  inazingatia  uwajibikaji wa watumishi wa umma  kwa wananchi na kujenga  utamaduni  wa kusikiliza na kutatua changamoto za wananchi moja kwa moja.

“Ninatambua uzito wa majukumu haya ya Uwaziri Mkuu pamoja na matarajio yake, pamoja na matarajio ya Watanzania. Nitafanya kazi kwa bidii, kwa uaminifu na jitihada kubwa kuweza kukidhi matarajio hayo,” amesema Dk. Nchemba.

Amesema  anatambua mahitaji  ya watanzania atasimamia kwa uadilifu na  jitihada  kuhakikisha  hayo yanatimia hivyo watumishi wa umma na watanzania wote kuwa tayari kuenda kwa gia ya kupanda mlima.

“Nawaonya Watumishi  wa umma  ambao ni wazembe,  wavivu na wala rushwa kujiandaa kukumbana na hatua kali  mara baada ya kuanza kazi rasmi na serikali haitavumilia urasimu,uzembe wala lugha za matusi  zisizofaa kwa wananchi, ” amesisitiza. 

Amesema  wananchi watasikilizwa  muda wote kwa heshima  kwenye ofisi zote za umma  lazima wawe waadilifu  na wenye kuwahudumia  wananchi  kwa wakati  kama anavyotaka Rais Dk.Samia. 

Ameongeza kuwa anataka kuona mabadiliko katika utendaji  wa watumishi wa umma hasa katika  utoaji wa huduma  kwa wananchi  ili kuhakikisha serikali  inatekeleza kwa vitendo  dhamira  ya kuwahudumia  Watanzania wote kwa haki na ufanisi.

“Natambua  matatizo ya ajira ya  kwa vijana natambua maumaumivu ya kukosa ajira hivyo naahidi kushirikiana kwa karibu  na Rais Dk.Samia  kuhakikisha  ajira  zinapatikana  na umaskini  unaokadiriwa kufikia asilimia  26 na unaupungua kwa kiwango  kikubwa  nchini,” amesema Dk. Nchemba. 

Akizungumzia kuhusu  Dira ya Maendeleo ya Taifa 2025-2050 amasema Dira hiyo imeweka kipaumbele kwenye masuala ya ajira ikiwa lengo ni kutoa ajira milioni nane kwa vijana nchini.

Amesema  Serikali  awamu  ya sita  inayoingia katika awamu  yake  ya pili kusimamia  utekelezaji  wa Dira ya Maendeleo ya Taifa  2025-2050 ambayo inalenga kuleta mafanikio makubwa  ya kiuchumi  na kijamii nchini.

Aidha amesema ameishi kwenye maisha ya umaskini kwa miaka 32, hivyo amewahakikishia Watanzania, hasa wenye maisha ya chini, kuwa watasikilizwa kwa nidhamu kwenye kila ofisi ya umma.

Dk. Nchemba amesema  maisha aliyowahi kupitia tangu akiwa nyumbani kwa baba yake yamekuwa ya msingi  wa dhamira yake ya kupambana na umasikini. 

Amesimulia jinsi alivyokulia katika mazingira magumu na hata baada  ya kuanza maisha ya ndoa na mkewe Neema waliendelea kukabiliana na  changamoto za  uchumi. 

“Spika, mimi  umasikini  nimeuishi nyumba kwetu tuliishi maisha ambayo shuka ya kujifunika ilikuwa ni kanga anayojifunga mama au dada yako na kama muvua  ikinyesha basi ngozi ndiyo unajifunika ili usilowane,”ameeleza Dk. Nchemba. 

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here