📌Aeleza Mkakati huo ni mwongozo wa kitaifa kwa wadau wote
📌Atoa wito kwa Maafisa dawati kuwa chachu ya mabadiliko ya Matumizi ya Nishati Safi ya Kupikia
📌Taasisi zilizo chini ya Wizara zaeleza zinavyotekeleza mkakati wa Taifa wa matumizi ya nishati safi ya kupikia
Na Mwandishi wetu, Mwanza
IMEELEZWA kuwa Mkakati wa Mawasiliano wa Nishati Safi ya Kupikia ni dira muhimu ya kufanikisha malengo ya Taifa ya kuhakikisha wananchi wanatumia nishati salama, rafiki wa mazingira na yenye gharama nafuu hadi kufikia mwaka 2034.

Hayo yameelezwa na Mwakilishi wa Mkurugenzi wa Kitengo cha Nishati Safi ya Kupikia Wizara ya Nishati, Mhandisi Banezeth Kabunduguru wakati wa kuhitimisha mafunzo kwa Maafisa Dawati na Waratibu wa Nishati Safi ya Kupikia wa Kanda ya Ziwa, yaliyofanyika jijini Mwanza Novemba, 142025.
Mhandisi Kabunduguru amefafanua kuwa, mkakati huo umekusudiwa kuwa mwongozo wa kitaifa utakaowaongoza wadau wote katika kutoa elimu sahihi, iitayofika kwa urahisi kwa wananchi wa makundi mbalimbali, ili kuongeza kasi ya matumizi ya nishati safi ya kupikia kama vile gesi (LPG), umeme, biogas na majiko banifu.
“Kwa kutumia mkakati huu, tunatarajia kuongeza uelewa wa wananchi kwa kiwango kikubwa na hivyo kupunguza utegemezi wa nishati isiyosafi unaochangia uharibifu wa mazingira na madhara ya kiafya. Huu ni mkakati wa mabadiliko na ninyi Maafisa Dawati ni nguvu ya mabadiliko hayo,” amesema Mhandisi Kabunduguru.

Ameongeza kuwa Serikali imejipanga kufanya kazi kwa karibu na Halmashauri, sekta binafsi, asasi za kiraia na wadau wa maendeleo kuhakikisha taarifa sahihi kuhusu nishati safi zinawafikia wananchi kwa wakati na kwa lugha inayowafaa.
Kwa upande wa Maafisa Dawati, washiriki wa mafunzo hayo akiwemo Dotto Masanja kutoka Karagwe na Christopher Kyamalesi kutoka Shinyanga, wameipongeza Serikali kwa kuandaa mkakati huo wakisema kuwa umetoa mwelekeo wa pamoja katika utoaji wa elimu kwa jamii.

Wameongeza kuwa, mkakati huo utawawezesha kuzungumza kwa sauti moja na kushirikiana kwa ufanisi na Viongozi wa vijiji, taasisi na wanajamii katika kuhamasisha matumizi ya nishati salama na kuondokana na matumizi ya kuni na mkaa.
Akizungumza kwa niaba ya Katibu Tawala wa Mkoa wa Mwanza, Aron Kalondwa amewataka Maafisa Dawati kutumia vyema mafunzo waliyopata na kuendelea kuwafikia wananchi wote kwa ubunifu na kujituma.
“Nishati safi ya kupikia si suala la Wizara pekee. Ni ajenda ya maendeleo ya Taifa. Elimu mliyopata leo inaweza kubadilisha maisha ya wananchi wetu na kupunguza Athari za kiafya na kimazingira”, Amesema Kalondwa.

Elimu hiyo imetolewa na Wizara Nishati kwa kushirikiana na Taasisi zilizo chini ya Wizara ambazo ni Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO), Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC), Wakala wa Nishati Vijijini (REA) ambazo zilieleza namna zinavyotekeleza mkakati wa Taifa wa matumizi ya nishati safi ya kupikia.
Aidha, Maafisa kutoka Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira na Ofisi ya Waziri Mkuu walitoa mawasilisho.
Mafunzo hayo yamehitimishwa leo Jijini Mwanza ambapo Mikoa iliyoshiriki mafunzo hayo ni Mwanza, Geita, Kigoma, Kagera, Shinyanga, Mara na Simiyu, ikiwa ni sehemu ya mpango wa Serikali wa kuongeza kasi ya uelimishaji kuhusu nishati safi ya kupikia katika mikoa yote nchini.



