📍Asema Waziri wa Nishati, Deogratius Ndejembi
📍Ni baada ya ziara yake kwenye vituo vya Gongo la Mboto, Kinyerezi I Extension na Mabibo
Na Mwandishi wetu, Dar es Salaam
WAZIRI wa Nishati M Deogratius Ndejembi amesema Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inayoongozwa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imewekeza zaidi ya Shilingi Bilioni 280 katika miradi mbalimbali ya umeme ili kuhakikisha upatikanaji wa uhakika wa nishati hiyo jijini Dar es Salaam.

Ndejembi ameyasema hayo Januari 6, 2025, wakati wa ziara yake katika vituo vya kupokea na kupoza umeme vya Gongo la Mboto, Kinyerezi I Extension na Mabibo vilivyopo jijini Dar es Salaam.
“Dar es Salaam ni miongoni mwa maeneo yanayotumia umeme mkubwa nchini. Ukiangalia uzalishaji wa umeme tulio nao, karibu megawati 750 zote zinatumika Dar es Salaam pekee. Uwekezaji huu uliofanywa na Serikali umelenga kuhakikisha uwepo wa umeme wa uhakika kwa watumiaji wa kawaida majumbani na viwandani ili navyo viendelee kukua,” amesema Ndejembi.
Aidha, amesema kuwa uwekezaji huo pia unalenga kuondoa utegemezi wa kituo kimoja cha kupoza umeme na badala yake kuwa na vituo vya kutosha vitakavyoondoa kabisa changamoto ya umeme pindi hitilafu inapotokea katika kituo husika.

“Lengo la Serikali kwa uwekezaji huu uliowekwa ni kuhakikisha katika Jiji la Dar es Salaam tunakuwa na ‘ring circuit’ (Mfumo wa umeme wa mzunguko) ili umeme unapokosekana upande mmoja, uweze kupatikana kupitia njia nyingine. Hii itawawezesha wakazi wa Jiji la Dar es Salaam na maeneo ya jirani kuwa na uhakika wa umeme muda wote,” ameongeza Ndejembi.
Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO, Lazaro Twange, amesema uwekezaji wa zaidi ya Shilingi bilioni 280 kwa Jiji la Dar es Salaam ni sehemu ya zaidi ya Shilingi trilioni 15 zilizotolewa na Serikali ya Awamu ya Sita katika kutekeleza miradi mbalimbali ya kuzalisha, kusafirisha na kusambaza umeme nchini.

“ Rais ametuelekeza, hataki kabisa sisi watu wa umeme tuonekane ndio kikwazo kwenye maendeleo ya watu. Tunamshukuru kwa kutuwezesha, na jitihada zote hizi zinaendelea kuhakikisha umeme unaendelea kuwa sekta wezeshi kwenye biashara, uwekezaji na utoaji wa huduma,” amesema Twange.

Ziara hii ya Waziri wa Nishati ni mwendelezo wa ziara zake za kutembelea miradi mbalimbali ya umeme nchini kwa lengo la kubaini maendeleo ya miradi hiyo na kuhakikisha inakamilika kwa wakati ili Watanzania waendelee kufurahia upatikanaji wa huduma ya umeme wa uhakika.



