Tehran, Iran
Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran, Abbas Araghchi, amesema kuwa taifa lake halina budi kujibu mashambulizi ya Marekani dhidi ya vituo vya nyuklia vya Iran, akisisitiza kuwa Marekani imevuka “mstari mwekundu mkubwa.”
Akizungumza na CNN, Araghchi alisema: “Wamevuka mstari mwekundu kwa kushambulia maeneo ya nyuklia… Tunapaswa kujibu kwa mujibu wa haki yetu halali ya kujilinda.”
Alipoulizwa iwapo Iran inazingatia kufunga Mlango wa Hormuz – njia muhimu ya maji katika Ghuba ya Uajemi inayotumiwa kusafirisha mafuta na gesi duniani – Araghchi alidokeza kuwa Iran ina “chaguzi mbalimbali mezani.”
Aidha, mwanadiplomasia huyo mkuu alieleza kuwa amekuwa akizungumza na mawaziri wa mambo ya nje wa nchi kadhaa za eneo hilo, ambapo amesema: “Karibu wote wana wasiwasi mkubwa na wana nia ya kuchukua hatua za kuzuia uchokozi wa Israel.”
Kauli hiyo imekuja wakati hali ya wasiwasi ikizidi kuongezeka katika Mashariki ya Kati kufuatia mashambulizi ya Marekani dhidi ya maeneo ya nyuklia ya Iran.