Na Mwandishi Wetu, Dodoma
KATIBU Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia masuala ya Sera, Bunge na Uratibu, Dk. Jim Yonazi amezitaka sekta zote kujianda kupokea wageni mbalimbali kuelekea Mashindano ya Mataifa ya Afrika (CHAN) yanatayorajiwa kuanza Mwanzoni mwa mwezi wa Agosti 2025.

Dk. Yonazi ametoa rai hiyo wakati akiongoza Kikao cha Makatibu Wakuu cha Tathmini ya Maandalizi ya CHAN na AFCON kilichofanyika leo tarehe 18 Julai, 2025 katika Ukumbi wa Ofisi ya Waziri Mkuu Jijini Dodoma.
Aidha, ameeleza kuwa jukumu la Serikali ni kuleta fursa na kuweka miundombinu ili kila sekta inufaike na ugeni huu mkubwa na kusisitiza hii ni fursa ya kutuamsha katika kuandaa matukio makubwa.

Pia, Dk.Yonazi amesisitiza umuhimu wa kutoa hamasa kupitia Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo ili kila mtanzania aamasike na kushiriki katika mashindano haya ya CHAN.

Ikumbukwe Mashindano ya CHAN yanatarajiwa kutimua vumbi kuanzia Agosti 2, 2025 ambapo timu ya Taifa ya Tanzania (Taifa Stars) itachuana na Timu ya Taifa ya Burkina Faso katika Uwanja wa Benjamin Mkapa Jijini Dar es Salaam.