Na Mwandishi wetu, Dodoma
MKURUGENZI Mkuu wa Mamlaka ya Udhibiti Mkundo wa Juu wa Petroli (PURA), Mhandisi Charles Sangweni amesema sekta ya kilimo na gesi asilia ni sekta zinazotegemeana kwa karibu.

Mhandisi Sangweni ameyasema hayo Agosti 7, 2025 alipotembelea Maonesho ya Kimataifa ya Kilimo ya Nane Nane yanayoendelea Jijini Dodoma amesema sekta hiziozikifungamanishwa vizuri zitaongeza tija katika uchumi.
“Gesi asilia inayozalishwa nchini inaweza kutumika kama malighafi kuzalisha ammonia, kemikali ambayo hutumika kuzalisha mbolea za aina mbalimbali ikiwemo urea,” amebainisha
Ameeleza kuwa, matumizi ya gesi asilia kwenye magari yamesaidia kupunguza gharama za uendeshaji hivyo gesi asilia ikitumiwa katika magari yanayosafirisha mazao ya kilimo, mifugo na uvuvi itasaidia kupunguza gharama za usafirishaji.

Kwa upande mwingine, Sangweni ameeleza kuwa sekta ya kilimo imeendelea kuwa nguzo muhimu katika utekelezaji wa miradi ya mafuta na gesi asilia kwa kulisha wataalamu wanaofanya kazi katika miradi ya mafuta na gesi asilia nchini.
Pamoja na sekta ya kilimo kutoa huduma hii muhimu, Sangweni alisema bado kumekuwa na changamoto kadhaa ikiwemo kampuni hususan kampuni za nishati za kimataifa kuhitaji bidhaa za kilimo zenye ubora na viwango ambavyo watoa huduma wachache wakitanzania wanakidhi.

Mhandisi Sangweni amebainisha kuwa, PURA kwa kushirikiana na wadau mbalimbali imeendelea kufanya jitihada za makusudi kuhakikisha kuwa viwango na ubora hitajika vinafikiwa kwa maslahi mapana ya uchumi.