Na Mwandishi wetu, Dar es Salaam
WAZIRI Mkuu Kassim Majaliwa amelipongeza Jeshi la Magereza Tanzania kwa kufanya urasimishaji wa ujuzi wanaoupata wafungwa kupitia VETA na kuwawezesha kupata ajira au kuanzisha biashara zao baada ya kumaliza kifungo.

Ameongeza kuwa kupitia mitaala mipya ya mafunzo ya amali na stadi za kazi, jeshi hilo limefanikiwa kuwanufaisha zaidi ya wafungwa 5,000 ambapo baadhi yao wameweza kujiajiri au kuajiriwa baada ya kumaliza vifungo vyao.
Ametoa pongezi hizo leo Agosti 26, 2025 wakati aliposhiriki katika maadhimisho ya kilele cha miaka 64 ya Jeshi la Magereza Tanzania yaliyofanyika katika viwanja vya Chuo cha Taaluma ya Urekebishaji Tanzania, Ukonga jijini Dar es Salaam.

“Ninatoa pongezi za dhati kwa jeshi la magereza kwa mafanikio haya, huu ni mpango kazi wenu, na tumeona faida na vijana hawa waliokuja hapa wameeleza namna ambavyo wamenufaika na kazi hizi,”amesema
Kwa Upande wake, Naibu Waziri wa Katiba na Sheria, Jumanne Sagini amelipongeza Jeshi la Magereza kwa wepesi katika kutafsiri na kutekeleza maelekezo ya Serikali na Viongozi mbalimbali na mengine bila kuwezeshwa fedha kutoka Serikalini.

Amesema, Jeshi hilo limeendelea kufanyia kazi mapendekezo yaliyotolewa na Tume ya Mhe. Rais ya kuboresha Vyombo vya Haki Jinai ikiwemo maboresho ya programu za urekebishaji wa wafungwa.
“Ujuzi wanaoupata wafungwa kutokana na mafunzo wanayoyapata yana umuhimu mkubwa katika kuwawezesha kufanya shughuli halali za kujikimu pale watakarudi kwenye jamii na hivyo kuwafanya kutorudia kutenda makosa.”

Awali, Kamishna Jenerali wa Jeshi la Magereza, Jeremiah Katungu amesema Jeshi hilo limefanikiwa kuandaa mitaala mipya 10 ikiwa ni hatua za kuboresha utoaji wa mafunzo stahiki kwa watumishi.
Amesema, Mitaala hiyo imeandaliwa kwa kushirikiana na Chuo cha Ustawi wa Jamii, Baraza la Taifa la Elimu ya Ufundi na Mafunzo ya Ufundi Stadi. (NACTVET), Tume ya Vyuo Vikuu Tanzania (TCU) na Taasisi ya Elimu ya Watu Wazima (TEWW).
“Tumeandaa Mwongozo wa Program za Urekebishaji kwa Wafungwa. Mwongozo huu umeweka misingi thabiti na utaratibu wa Mapokezi, Tathmini, Urekebishaji na kuwaandaa wafungwa kurejea kwenye jamii wakiwa raia wema,”amesema.