Home SIASA Mbeto:Rais Dk Mwinyi kutekeleza ahadi zote bila longolongo Zanzibar

Mbeto:Rais Dk Mwinyi kutekeleza ahadi zote bila longolongo Zanzibar

Na Mwandishi Wetu,Zanzibar

CHAMA cha Mapinduzi kimewatoa hofu Wazanzibari kuwa ahadi zote za kisera zilizoainishwa katika Ilani ya Uchaguzi ya CCM 2025-2030 zitatekelezwa na Rais wa Zanzibar Dk Hussein Ali Mwinyi bila longolongo.

Pia chama hicho kimesisitiza CCM kitasimama kama manyapara ili kuhakikisha kila ahadi inatimizwa kwa wakati .

Matamshi hayo yametamkwa na Katibu wa Kamati Maalum ya NEC Zanzibar, Idara ya Itikadi ,Uenezi na Mafunzo ,Khamisi Mbeto Khamis mbele ya waandishi wa habari baada ya kumalizika Kikao cha Kamati Maalum ya NEC Zanzibar.

Kikao hicho cha Kamati Maalum ya NEC Zanzibar, kimekutana chini ya Makamo Mwenyekiti wake, Rais Dk Mwinyi katika Afisi Kuu ya CCM,Kisiwandui mjini Unguja.

Mbeto amesema Msimamizi namba moja wa utekelezaji wa sera za chama ,ni chama chenyewe , ambacho kitafuatilia kila sekta na kuhakikisha ahadi zote zimetekelezeka.

Amesema baada ya wataalam wa chama kuandika ilani , hatimae ikapitishwa na mkutano Mkuu wa Taifa wa CCM ,kazi ya usimamizi na ufuatiliaji itabaki mikononi mwa vongozi wa chama kuanzia matawi hadi Taifa.

“Napenda niwatoe hofu Wazanzibari kupitia kwenu wana habari.Kazi ya utekelezaji wa ahadi itafanywa na chama katika ngazi zake. Kwa utekelezaji wa Sekta za Umma kazi itafanywa na watendaji wa SMZ,” amesema Mbeto

Aidha, Katibu huyo Mwenezi aliongeza kusema kuwa CCM ndicho kilichoshinda Uchaguzi Mkuu,kina ridhaa ya wananchi hivyo kaz iliobaki ni kuhakikisha inasimamia utekelezaji wa sera zake .

“Tutapita kila kona ya sekta za umma kufuatilia utekelezaji wa ahadi . Tukikuta mahali mambo hayaendi tunavyotaka tutaziarifu Mamlaka husika zichukue hatua stahiki,”ameeleza

Katibu huyo Mwenezi alisema sababu ya CCM kupata ushindi wa kishindo, imetokana na utelelezaji makini,usio na urasimu wala ngojangoja katika miaka mitano iliopita.

“Wananchi wanapoahidiwa ahadi wangependa kuona matokeo ya ahadi hizo zikitekelezwa na serikali yao si jambo jingine,”amesisitiza Mbeto .

Mbeto ametoa wito kwa wabunge,wawakilishi na madiwani wa CCM kuhakikisha wanatimiza ahadi za kisera na zaki binafsi kwa muda na wakati bila kutoa visingizio.

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here